ONLINE

Tuesday 18 October 2022

Afadhali Jadi


AFADHALI JADI



By Calson Mugodo

             Ewe Mola mraufu, mie mja wako mwenye mapungufu nina tamanio na ombi mtimani, ninaomba kwa taadhima nirejeshwe jadi walipo mababu zangu.

             Naam, zamani kusiko na runinga wala rununu, nisifahamu jambo kuhusu kipakatalishi wala kiotomotela. Huko jadi sitahitaji senti ili kuyakidhi mahitaji yangu. Iwapo itanipasa nife ili nirejee jadi, basi nipo radhi kufa, Yarabi, mtume Israili mtoa roho aniburure waama anibebe hobelahobela hadi kule.

           Natamani kukutana naye babu ya babu yangu, nisiyemfahamu hata jina, nikiulizwa kisa na sababu eti nilikuwa nikihangaika na madaftari shuleni nisipate muda wa kusikiliza hadithi kutoka kwa babu kumhusu babu yake. Ninataka kustarehe kwenye kifua kipana cha babu ya babu yangu, kilichojaa  vinyweleo huku nikiusikiliza taratibu wimbo wa utamaduni unaomtoka kinywani, huku mjomba aliye stadi wa kupiga ngoma, siku hizi twamuita sogora akitekeleza wajibu wake.

           Nataka kwenda jadi ambako ndwele kama vile kansa na UKIMWI ni visa vya kufikirika. Angecheka sana babu iwapo ningemweleza kuwa binadamu anaweza kudhoofika akakonda na kukondeana kiasi cha mbavu zake kuhesabika ubavu baada ya mwingine kutokana na makali ya UKIMWI. Na iwapo maradhi kama haya yangetokea, hofu haingekuwepo kwani penye wazee hapaharibiki jambo, wazee wenye hekima wangekusanyika usiku wa manane ama alfajiri ya majimbi ili kujadili suluhu mwafaka, kisha wangejitoma mwituni au pangoni na kumtoa kafara beberu kwa mizimu kwa ajili ya taambiko. Kisha wangefanya wanavyojua wao mpaka mizimu iwaelekeze palipo majani au mizizi iliyo tiba kwa ugonjwa huo.

           Kule jadi swala la ndoa lilikuwa muswaki. Wanapobalehe maghulamu, wangeelekezwa moja kwa moja hadi jandoni, kisha ngariba angeruhusiwa kuutekeleza wajibu wake. Kisha wangesalia kule kwa muda wa takribani miezi sita bila kurejea nyumbani. Wangefundishwa majukumu ya mwanamume na jinsi ya kuishi na wake zao vile vile namna ya kujitegemea na kutafuta riziki kwa kuwinda wanyama pori na kupitia zaraa. Kijiji kizima kingetumbuizwa kwa nyiso zinazoimbwa kila usiku na mashujaa hao walio jandani. Mwana wa mtu anapotoka jandoni akiwa kwenye pita pita zake, kwenye baraste angekutana na mwanamwali mrembo kutoka utosini hadi kwenye vidole vya mguu , ghulamu aliyekomaa tayari kuuasi ukapera angemtamani nusra mate yamdondoke . La kufurahisha ni kwamba mwanamume huyu asingejisumbua kumshawishi binti huyu aliyefunzwa unyagoni akaelewa somo, badala yake angehitaji tu kuzungumza na abu yake, kisha washenga wangetafutwa kupeleka posa kwa wazazi wa binti. Kisha kungefuatia harusi ya kiasili baada ya mahari kulipwa , kisha wazee wangebugia mvinyo maalum kama ishara ya makubaliano na ushirikiano. Tena takriban mabinti wote walikuwa mabikira hadi wakati wa ndoa, ni raha iliyoje? Huko ndiko ninakotaka kwenda.

             Natamani kuwa pamoja na wazee wangu kando ya miale ya moto, tena moto uliowashwa kwa kuzungusha kipande cha mti juu ya gogo hadi moto ukatoka bila kutumia kiberiti. Kisha babu angechukua hatamu na kutamba hadithi zenye mashiko moja baada ya nyingine mpaka mtima uridhike na kusema tosha. Baadaye tungejikunyata ndani ya jamvi lililotengenezwa kwa ngozi ya ng'ombe ili angalau tupate usingizi.

             Iwapo kungetokea mwizi usiku huo, akanyatia nyatunyatu na kumchukua ng'ombe mmoja, Babu angeiamkia mizimu na kufanya anavyojua yeye mpaka yule mwizi amrejeshee ng'ombe na kuomba msamaha. Kisha babu angemsamehe kwani anafahamu fika ubaya hauondolewi kwa ubaya ila wema, kwa hivyo, angempa ushauri na maelezo kindakindaki ya jinsi ya kujitafutia mali yake mwenyewe.

           Nikiwa kule sitavitamani vyakula vya huku kwenu kama vile sharubati na vibanzi , badala yake nitaridhika na kutafuna minofu ya nyama iliyochomwa na kufukizwa kwa moshi pamoja na vyakula vya kiasili ikiwemo mizizi na majani ya mimea ainati yenye uwezo wa kukabiliana na magonjwa yote. Nakomea hapo kwa sasa nitaiendeleza hadithi hino nikirejea kutoka jadi.

                    

     

 

No comments:

Post a Comment