ONLINE

Sunday 12 March 2023

Mashetani Wekendu wageuzwa kitoweo “Anfield”

 



Na Jeremiah

Baada ya msururu wa ushindi wa mechi kadhaa bila kusahau kutwaa kombe la Carabao jumapili iliyopita,hatimaye  Manchester United    wapokea kipigo  kilichowaacha wengi vinywa wazi.Hiki ndicho kipigo kikubwa zaidi kunakiliwa msimu huu katika ligi kuu ya Uingereza .Vilevile,  ilikuwa historia hasi kunakiliwa  kwa upande wa Manchester United katika karne ya ishirini na moja .

Kambi yote ya wababe hawa wa Ulaya ilionekana kutoyaamini macho yao  toka kwa mkufunzi wa hapo awali , Sir Alex Ferguson hadi mkufunzi wa sasa ,Eric Ten Hag ambaye bado alikuwa mgeni katika ligi kuu ya Uingereza. Kwingineko, nyuso za mashabiki wa Manchester united zilisheheni soni na ghadhabu dhihirisho wazi la kutamaushwa na matokeo hayo.

Upande wa pili, ilikuwa furaha si haba miongoni mwa kikosi cha Liverpool kwani, kila mshambulizi aliyesajiliwa msimu huu alizitikisa nyavu mara si moja; sisemi Darwin Nunez bali pia Gakpo . Pamoja nao walikuwa mashabiki  wa timu zenye uhasama na Manchester united; hii ni ikiwemo Arsenal, Chelsea na Manchester city ambao waliusherehekea ushindi huo kote nchini sisemi mitandaoni,katika vyumba vinavyouzwa vileo na hata vyuoni ungedhani timu zao ndizo zilizoshinda.

Timu zote zilionekana kutoshana  nguvu dakika arubaini za kwanza.Aidha,ngome ya ulinzi ya Manchester United  ilishindwa kustahimili makali ya washambulizi wa Liverpool .Baada ya  kulaza damu katika dakika ya arubaini na  mbili , Cody Gakpo alitia wavuni bao lililowaweka Liverpool kifua mbele katika kipindi cha kwanza.Hapo awali Marcus Rashford alikuwa keshapata nafasi ya kucheka na wavu ila mlindalango wa Liverpool alionyesha umahiri wake kwa kulinyaka shoti hilo kwa urahisi.

 



Licha ya Wout Weghorst na Diogo Dalot kuonyesha mchezo wenye kiwango cha chini,Ten Hag alionekana kuwa na imani nao kipindi cha pili kwani hakufanya badiliko lolote la kuwatoa mwanzoni mwa kipindi cha pili.

Kipindi cha pili kilipong’oa nanga ,dakika hazikuzidi tatu Liverpool wakaongeza bao la pili kupitia kwa mshambulizi Darwin Nunez .Kila kiungo cha Manchester United  wakati huu kilionekana kujisahau kwani dakika ya hamsini  Cody Gakpo aliongeza bao lake la pili na  kuifanya timu yake kuongeza ushindi wao kwa mabao matatu bila jawabu.


Kadri muda ulivyoyoyoma mbinu za mibabe hii kutoka jiji la Manchester zilionekana kulemaa na hivyo kumlazimu Mkufunzi wao kufanya mabadiliko mawili dakika ya  hamsini na nane. Hata baada ya mabadiliko hayo,wapinzani wao walionekana kuwazidi katika safu zote si ushambulizi tu bali pia viungo.

Kama ilivyo ada yake, Mohammed Salah aliyafichua makucha yake dakika ya sitini na sita alipofyatua kombora lililomwacha De Gea hohehahe na hivyo kuongeza idadi ya mabao hadi manne. Wana Liverpool walionekana kutotosheka  na mabao kwani dakika tisa baadaye , Henderson,kiungo wa Liverpool alimmegea Darwin Nunez krosi ambayo Nunez alitumia kichwa chake kuiunganisha na kucheka na wavu kwa mara ya pili.

Liverpool walifanya mabadiliko yao dakika ya sabini na nane, sabini na tisa na themanini na tano mtawalia. Wapinzani wao kwa upande mwingine walimalizia mabadiliko yaliyosalia dakika ya sabini na saba na themanini na tano mtawalia.

 

Mnamo dakika ya themathini na tatu ,Salah alitia kimiani bao la sita alilolisherehekea kwa kuivua  jezi yake.Tukio hili lilimfanya aadhibiwe kwa kupewa kadi ya manjano.Dakika mbili kabla ya mechi kutamatika,Roberto Firmino aliyekuwa mchezaji wa akiba alitamatisha karamu ya mabao kwa kufunga bao la saba.

“Wasio na taaluma.”Ten Hag alithibitisha katika uchambuzi wa baada ya mechi . Kipindi cha pili kilikuwa dhihirisho wazi wa aliyoyasema Ten Hag. Kikosi chake kilikosa dira ama kwa uhakika. Walishindwa kuidhibiti kasi ya  mchezo  kinyume cha wapinzani wao walioonekana kuwa watulivu licha ya shinikizo kutoka kwa washambulizi kama Marcus Rashford. Baadhi ya wachezaji walionyooshewa vidole kwa kuchangia ushinde huo ni pamoja na Wout Weghorst,Diogo Dalot,Luke Shaw na Rafael Varane.

 

No comments:

Post a Comment